Loading...

Tukubaliane, hatuna wimbo wa taifa

Mwalimu Julius Kambarage NyerereKUMEKUWAPO na mjadala kwamba Watanzania hatuna wimbo wa taifa. Mjadala huu upo ndani na nje ya nchi yetu. Unashirikisha Watanzania na wasio Watanzania, anaandika Ansbert Ngurumo.
Kuhusu suala hili, nakumbuka niliwahi kubanwa na baadhi ya raia wa Swaziland na Lesotho, mwaka 2001 nikiwa jijini Mbabane kwa mafunzo mafupi ya uchambuzi wa kisiasa.
Ilianza kama utani tu, lakini ikaishia kwenye mjadala mpana, ambao hakuna aliyekubali kushindwa.
Tulikuwa kundi la waandishi wa habari kutoka nchi mbalimbali za Afrika Kusini mwa Sahara. Watanzania tulikuwa wawili – mimi, na Mayage S. Mayage, wakati huo nikiwa naandikia magazeti ya The African na Rai.
Katika shamrashamra za hapa na pale, siku moja wakati wa mapumziko, mmoja wa washiriki wa mafunzo hayo, raia wa Lesotho, akapendekeza kila watu waimbe wimbo wao wa taifa. Likaonekana ni jambo jema, kila mtu ajivunie utaifa wake na nchi yake mbele ya wenzake.
Kila wimbo ulipoimbwa, ulihitimishwa kwa makofi ya shangwe na (wakati mwingine) vigelegele kutoka kwa akina dada waliokuwapo. Tulikuwa tunaimba kwa mzunguko. Ilipofika zamu ya Tanzania, tukaanza kuimba kwa mbwembwe.
Hatukumaliza hata ubeti wa kwanza. Mara tukakatizwa na mmoja wa wasikilizaji wetu, akisema, “samahani, tumesema Tanzania. Sasa mbona mnaimba wimbo wa Afrika Kusini? Hamjui utaifa wenu nini?” Kabla hatujajibu, mwingine akadakia: “Hapana, huu wimbo ni wa Zambia. Hebu tuimbieni wimbo wenu.” Wengine wakacheka kama vile wanataka kutuzomea.
Nikakaribia kuwakasirikia, lakini nikawaeleza kwa upole kuwa hoja zao zinaonesha walivyo “washamba” kwa kushindwa kujua kuwa tunachoimba si wimbo wa Afrika Kusini wala wa Zambia, bali wa Tanzania. Nikawaeleza kwamba wangetuacha kwanza tukaumaliza ndipo waufananishe na hizo wanazozungumzia.
Nikawataka waelewe kwamba nyimbo kufanana tuni si kosa, bali ni sehemu ya, na zao la, umoja wa dhamira ya mapambano na ukombozi wa bara letu.
Nikasema kuwa na wimbo unaofanana ni sifa si kejeli; ni kama kuwa na lugha moja inayowafananisha Waafrika na kuonesha udugu na mshikamamo ambao Waafrika wanahitaji sasa, labda kuliko wakati wowote wa historia yao.
“Sawa. Lakini haiondoi kwamba wimbo huo unajulikana ni wa Afrika Kusini. Nyie mmeunakili. Mna hakimiliki?” Alihoji mmoja wao.
Hata hivyo walio wengi waliona mantiki katika hoja yangu ya “kulazimisha.” Nililazimisha hoja hiyo kutetea wimbo wetu, kwa sababu sikuwa na sababu ya kuonesha unyonge wa Watanzania mbele ya raia wa nchi nyingine.
Nilitimiza azima hiyo, lakini dhamiri yangu ilikuwa inaniambia kwamba, “vijana hawa wana hoja.” Bahati niliyokuwa nayo ni kwamba sikukutana na mmoja wao mwenye hoja kali.
Walikuwa na ubishi tu, na waliridhika haraka haraka na maelezo yangu ya juu juu na ya kulazimisha. Labda mjadala ungekuwa mkali na mrefu kama wangehoji zaidi, maana sikuwa tayari kushindwa kueleza kwa nini Watanzania hatuna wimbo wetu.
Hoja hii imekuwa ikijadiliwa pia na baadhi ya wanasiasa wetu, hasa walio katika vyama visivyo madarakani.
Nakumbuka kipindi fulani, akina Bob Makani (wakati huo akiwa Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo) na Freeman Mbowe (katika awamu ya kwanza ya ubunge wake wa Jimbo la Hai), waliwahi kuvalia njuga suala la wimbo wa taifa.
Wapo baadhi ya wanaharakati, wakiwamo waandishi wa habari, walikubaliana nao. Sababu ni zile zile kwamba hatuna wimbo wetu. Tumeazima.
Walifika mahali pa kusema kwamba, Chadema kikiingia madarakani, watabadili wimbo wa taifa kwa sababu huu uliopo hauna mvuto na hausisitizi utaifa. Wakapendekeza tubadili wimbo, badala ya huu wa sasa, tuimbe “Tanzania, Tanzania, nakupenda kwa moyo wote…”
Naamini viongozi wetu, kama ilivyo kawaida ya viongozi wa Afrika, waliona suala hilo ni la wapinzani, na ni la kipinzani.
Sijawahi kusikia viongozi wetu wakilijadili. Sijawahi kusikia hata mbunge mmoja wa CCM akinukuliwa kutoa hoja hiyo kwenye vikao vya uamuzi.
Na zikiimbwa nyimbo zote mbili (Mungu Ibariki Afrika; na Tanzania nakupenda kwa moyo wote), ni dhahiri kwamba huu wa pili ndio unasikika na kuhisiwa wa kizalendo kwetu. Ni wimbo wetu.
Zaidi ya hayo, kwa sababu ya ukubwa wa Afrika Kusini na umaarufu wake katika dunia, wimbo wake umefunika wimbo wetu. Siku zikutanapo timu za taifa, au viongozi wetu wanapotembeleana, zikipigwa nyimbo hizo, ndipo ukweli huu unapogundulika. Tumeiga.
Kwa faida tu ya wasomaji, ngoja nieleze historia fupi ya wimbo huu. Katika dunia nzima, hasa Afrika Kusini kwenyewe ulikoanzia, unajulikana kama “Nkosi Sikelel’ iAfrika” – maneno ya lugha ya ki-Xhosa, yenye maana ya “Mungu Ibariki Afrika.”
Mtunzi wake anaitwa Enoch Sontonga, aliyekuwa mwalimu katika shule moja ya misheni ya Kimethodisti, Johannesburg, Afrika Kusini.
Aliutunga ukiwa kama utenzi mwaka 1897. Uliimbwa kwa mara ya kwanza hadharani mwaka 1899 katika ibada ya kuwekwa wakfu mchungaji Boweni, wa Kanisa la Methodist.
Kwaya ya Sontonga na kwaya nyinginezo zikawa zinauimba mara kwa mara katika matukio jijini Johannesburg na Natal. Watu wakaupenda.
Mnamo Januari 8, mwaka 1912, katika mkutano wa kwanza wa Chama cha Wazawa wa Afrika Kusini (SANNC), mtangulizi wa ANC, wimbo huo uliimbwa mara baada ya sala ya kufunga mkutano.
Mwaka 1925, ANC ikauchukua kama wimbo wake rasmi ulioimbwa mwishoni mwa mikutano yake. Tangu hapo, wimbo huo umejulikana nje ya Bara la Afrika kama wimbo wa ANC, kwani ulikuwa ukiimbwa katika mikutano ya ANC katika harakati za ukombozi.
Harakati hizo ndizo zilifikisha wimbo huo hadi kwetu. Nasi tulipopata uhuru, tukauchukua kama wimbo wa taifa, tukautafsiri kwa Kiswahili, tukapunguza baadhi ya aya na kuubakiza kama ulivyo leo.
Zambia nao walifanya hivyo. Namibia pia waliutumia. Zimbabwe nao waliuiga, lakini baadaye “walipopata akili” wakautema, wakatunga wimbo wao.
Kwa kipindi kirefu, Afrika Kusini ilikuwa na “nyimbo mbili za taifa.” Mmoja ulijulikana kama wimbo rasmi na mwingine, usio rasmi.
Wimbo rasmi (uliotumiwa na serikali ya makaburu) uliitwa kwa jina la Die Stem (ki-Afrikaans), yaani Wito wa Afrika Kusini; na usio rasmi (uliotumiwa za wanaharakati wa ANC), ndio huo Mungu Ibariki Afrika.
Siku ANC iliposhinda uchaguzi wa kwanza kidemokrasia mwaka 1994, nyimbo hizo mbili zikatangazwa kuwa nyimbo rasmi za taifa, lakini mwaka 1996 ziliunganishwa; yakachukuliwa maneno huku na huku, ghani ikabaki ile ile ya wimbo wa ANC, ukakarabatiwa na kuwa kama ulivyo leo.
Kwa Afrika Kusini, Nkosi Sikelel’ iAfrika, kabla na baada ya uhuru, ni ishara ya uhuru na mapambano ya ukombozi wao. Unaimbwa katika lugha mbalimbali Kixhosa, Kiingereza, Kisesotho na Kiafrikaans.
Maneno yaliyo katika aya ya kwanza yaliandikwa na mtunzi mwenyewe (Enoch) katika lugha yake ya Xhosa. Mwaka 1927, aliyekuwa mmoja wa washairi maarufu wa nchi hiyo, Samuel Mqhayi, aliongeza aya nyingine saba katika lugha hiyo hiyo.
Kabla ya hapo, mwaka 1923, Solomon Plaatje, mmoja wa waandishi mahiri nchini humo, ambaye pia alikuwa miongoni mwa waasisi wa ANC, ndiye alikuwa mtu wa kwanza kuurekodi wimbo huo katika studio jijini London, akisindikizwa na muziki wa piano uliopigwa na Sylvia Colenso.
Mwaka huo huo, kiwanda cha uchapaji cha Lovedale Press, katika Jimbo la Eastern Cape, kilichapisha nakala yenye aya zote katika kijitabu. Juni 11, 1927, wimbo huo ulichapishwa katika gazeti la Umtetela Wa Bantu, ukaingizwa pia katika kitabu cha ushairi cha Kixhosa kwa ajili ya kuwafundishia watoto shuleni.
Wimbo huo pia uliingizwa rasmi katika kitabu cha nyimbo za Kixhosa kwenye Kanisa la Wapresbyteri kilichojulikana kama Ingwade Yama-culo Ase-rabe, mwaka 1929. Mwaka 1942, Moses Mphahlele, alichapisha nakala nyingine za wimbo huo katika lugha hiyo na kuzisambaza ili umma ukariri vema maneno yake.
Kwaya ya Ohlange Zulu, ya Mchungaji John L. Dube, ndiyo iliyokuza wimbo huo, kwa kuuimba mara kwa mara katika matamasha mbalimbali jijini Johannesburg.
Taratibu ukawa wimbo maarufu katika mikusanyiko ya kidini, kijamii na kisiasa; badaye ukarekodiwa pia na wasanii kina Ladysmith, Black Mambazo, Boom Shaka na Mahotella Queens.
Historia hiyo pekee inaonesha kwamba sisi bado hatuna wimbo. Kama tunavyoimbiwa na wasanii wa CCM kwamba “CCM ina wenyewe,” basi tuna sababu ya kuamini pia kwamba hata wimbo huu tunaouita wa taifa, una wenyewe – na wenyewe ni Afrika Kusini. Nadhani Wazimbabwe waliligundua hilo mapema. Wakaachana nao. Sisi tunangoja nini?
Ni bahati mbaya kwamba vijana wale waliobishana nami hawakuwa wanajua historia ya wimbo huo kama nilivyoieleza hapa. Vinginevyo, walikuwa na hoja; na wangetuaibisha. Tuna wasanii wa kutosha kutunga nyimbo zetu.
Watunge. Kama hatutaki mpya, basi tuchukue zilizopo, zinazoeleza kwa kina historia na utaifa wetu, tuzifanye rasmi nyimbo zetu za taifa, kwani huu tunaoimba sasa si wimbo wetu.

Post a Comment

CodeNirvana
Newer Posts Older Posts
© Copyright CHACHANDU | Designed By AFROPIXELS MEDIA CO. LTD
Back To Top