Loading...

Mchakato wa kumrithi Lipumba wakolea

Aliyekuwa Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi CUF, Prof. Ibrahim LipumbaCHAKATO wa uchaguzi mdogo ndani ya chama cha wananchi (CUF) umeendelea kushika kasi ambapo uchukuaji wa fomu za kuwania nafasi ya Mwenyekiti wa chama hicho iliyoachwa wazi na Profesa Ibrahim Lipumba unaendelea, anaandika Charles William.
Zoezi la ugawaji wa fomu za kuwania nafasi hiyo linaendelea ambapo wanachama wa CUF wanachukua fomu kupitia ofisi za chama hicho ngazi ya Wilaya huku baadaye fomu hizo zikitarajiwa kukusanywa zote na kupelekwa ngazi ya taifa.
“Fomu zipo wilayani, wanachama wanaojiona wana uwezo wa kushika nafasi husika wanachukua fomu na kurejesha ofisi za CUF wilaya na tunapata taarifa kuwa zoezi linaenda vizuri, watu wengi wanazidi kujitokeza.” Ameeleza Shaweji Mketo Mkurugenzi wa uchaguzi CUF.
Akizunguma katika mahojiano maalum na Mwanahalisionline, Mketo amefafanua kuwa zoezi la kuchukua na kurejesha fomu lilianza tangu tarehe 1 Julai mwaka huu na linatarajia kufikia tamati 20 Julai mwaka huu.
“Baada ya watu kurejesha fomu kuanzia 21 Julai mpaka 30 Julai kamati tendaji za CUF ngazi ya wilaya zitafanya uchambuzi wa majina hayo na sisi chama ngazi ya taifa tutayapokea rasmi majina ya wagombea na fomu zao kuanzia 1 Agosti 2016. Ameongeza Mketo.
Kuhusu idadi na majina ya wanachama wa CUF waliochukua fomu za kuwania nafasi ya uwenyekiti mpaka sasa, Mkurugenzi huyo wa uchaguzi, amesema bado chama hicho ngazi ya taifa hakina taarifa rasmi za idadi na majina ya wagombea kwani zoezi linaedeshwa wilayani.
Lipumba alijiuzulu uwenyekiti wa CUF Agosti mwaka jana, kwa kile alichokiita “nafsi kumsuta” kufuatia mwanasiasa Edward Lowassa kuhamia CHADEMA na kuidhinishwa kuwania urais kwa niaba ya vyama vya umoja wa katiba ya wanachi (UKAWA).
Hata hivyo mwezi Juni, mwaka huu profesa Lipumba alijitokeza na kudai ameandika barua kwenda kwa Katibu Mkuu wa CUF taifa, Seif Shariff Hamad akiomba kuirejea nafasi yake, ombi ambalo linaonekana kutupiliwa mbali kufuatia CUF kuanza kwa ugawaji wa fomu za kuwania nafasi hiyo  mapema mwezi huu.

Post a Comment

CodeNirvana
Newer Posts Older Posts
© Copyright CHACHANDU | Designed By AFROPIXELS MEDIA CO. LTD
Back To Top